John Mapepele Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Mohamed Mchengerwa ameipongeza Kampuni ya Wasafi kwa kukuza sanaa ya muziki na kuzalisha ajira kwa vijana wengi hapa nchini. Akizungumza kwenye hafla ya Usiku wa Mahaba Ndi Ndi Ndi siku ya wapendanao Februari 14, 2022 jijini Dar es Salaam amesema Wasafi ina mchango mkubwa katika kuibua na kukuza vipaji vya wanamuziki. " Naomba nikuhakikishie Serikali ipo pamoja na nyie katika kukuza sanaa " amesema Mhe.Mchengerwa Aidha, amesema Serikali inakwenda kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Wasafi mtaa kwa mtaa, kijiji kwa kijiji hadi mkoa kwa mkoa kutafuta vipaji vya wasanii lengo ni kuwashindanisha na kuwaendeleza. Ameongeza kuwa, wizara inakwenda kuendeleza mapinduzi ya ukuzaji wa Sanaa ili kutoa ajira zaidi kwa vijana katika ngazi ya kitaifa na kimataifa. Amefafanua kwamba kufanya hivyo ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya kutaka kuboresha sekta hiyo ili wasanii nchini waweze kunufaika na kazi zao. Kwa upande mwingine Mhe. Mchengerwa amesema, katika kipindi hiki sanaa inakwenda kutumika kuitangaza Tanzania kimataifa. Naye Mtendaji Mkuu wa Wasafi, Msanii nguli wa muziki wa kizazi kipya barani Afrika, Diamond Platinum ameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga mazingira wezeshi kwenye Sekta ya Sanaa nchini. Waziri Mchengerwa akitoa salamu za Serikali kwenye usiku wa Mahaba ndi ndi ndi Mtendaji Mkuu wa Wasafi na Msanii nguli Afrika Diamond Platinum akiongea kwenye Usiku wa Mahaba ndi ndi ndi Februari 14, 2022 Katibu Mkuu, Dkt. Hassan Abbasi akiwatambulisha Mawaziri wanaosimamia Sanaa na Habari kwenye usiku wa Mahaba ndi ndi ndi Februari 14, 2022 Mwanamuziki Zuchu akitumbuiza katika Usiku wa Mahaba ndi ndi ndi Februari 14, 2022.

 Na. John Mapepele

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa leo Februari 14, 2022 ametoa maelekezo mazito kwa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) na Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) yanayolenga kuboresha mchezo wa mpira wa miguu nchini.

Maelekezo hayo ameyatoa katika mkutano wa Waandishi wa Habari aliofanya katika Ukumbi wa Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam leo Februari 14 baada ya kufanya kikao na Viongozi wa TFF, BMT na watendaji wa Wizara.

Amefafanua kuwa Serikali ipo katika mikakati kabambe ya kuboresha miundombinu ya michezo katika shule 56 nchini ikiwa ni pamoja na kufunga mashine za kisasa za kufuatilia michezo (VAR) kwenye  viwanja vitano  kwa kuanzia pamoja na kujenga  vituo  vikubwa vya michezo.

Akitoa  maelekezo ya Serikali,  Mhe. Mchengerwa amesema BMT likutane na TFF mara moja kujadili namna ya  kudhibiti vitendo  vya  ukiukwaji wa Sheria na taratibu za mchezo huo pendwa nchini ambapo pia amesisitiza  kuwa Kamati inayohusika na Waamuzi ijitafakari kwa kuwa hadi sasa kwenye msimu huu wa ligi tayari imeshawaondoa waamuzi 13 kwa makosa ya upendeleo na rushwa.

Pia amesema TFF likutane na waamuzi wote ili kupata uvumbuzi wa changamoto na sintofahamu zinazoendelea kujitokeza katika mchezo huo kinyume na sheria ambapo TAKUKURU washirikishwe wawepo ili waweze  kutoa elimu ya rushwa  kwenye mchezo wa mpira wa miguu.

Amefafanua kuwa iwapo Serikali  haitaweza kudhibiti vitendo vya rushwa kwenye mchezo wa mpira wa miguu, mchezo huo  hautakuwa na maendeleo.

Aidha, amesisitiza waamuzi wasio na sifa waondolewe moja kwa moja  na kuwaleta wengine  wenye sifa na   TFF lihakikishe utekelezaji wa sheria na kanuni za vilabu huku BMT iendelee kusimamia  utawala bora ili kuwe  na ustawi  katika michezo.

Pia ameviomba Vyombo vya Habari kuelimisha jamii  kuhusu programu mbalimbali za redio na televisheni kuhusu sheria za mpira wa miguu kupitia kwa wakufunzi na waamuzi.

Katika  mkutano huo Mhe. Mchengerwa aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara yake Dkt. Hassan Abbasi, na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya michezo na Kaimu katibu Mtendaji wa Baraza la Michezo la Taifa(BMT) na   Uongozi wa TFF



Comments

Popular posts from this blog

Mhe. Mchengerwa Atoa salamu Siku ya Afrika

RAIS SAMIA AANZA NA WAANDISHI WA HABARI